Jumla ya wahudumu wa afya 35 mkoani Mara wamepata mafunzo ya afya kutoka shirika la afya la AGPAHI kwa kushirikiana na wizara ya afya, Maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto kupitia mpango wa kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto aliyezaliwa na mama mwenye VVU.
Akizungumza wakati wa ufunguaji wa mafunzo hayo mgeni rasmi ambaye ni mganga mkuu wa mlkoa wa Mara Dk. Florian Tinuga, aliwataka wahudumu wa afya kupokea mafunzo hayo ya mfumo mpya ili kuhakikisha maambukizi mapya hayatokei katika vituo vya kutolea huduma ya afya.
"hakikisheni mnapitia kile mlichojifunza kwa umakini na kuyafanyia kazi kwa weledi kwani jamii inawategemea sana hata taifa kwa ujumla" amesema Dk. Tinuga.
Naye mkufunzi katika warsha hiyo Alvera Pangani, amesema kuwa mafunzo hayo ni endelevu na wataanza kufuatilia kwa kila mshiriki kwa kupata taarifa sahihi kile alichojifunza kama kimefanyiwa kazi vyema, ikiwemo kutatua changamoto za watoa huduma za afya.
Pia amewaasa watoa huduma za afya kuwasilisha taarifa wilayani za mama wajawazito na wanaonyonyesha wenye maambukizi ya virusi vya Ukimwi pamoja na watoto kila baada ya tarehe 5, Juni kila mwaka.
Aidha katika kuimarisha utekelezaji wa mfumo huo, Shirika la AGPAHI, linatoa mafunzo ya watoa huduma za afya kutoka katika vituo vya kutolea huduma za afya katika Mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Mara na Simiyu.